KATIKA hali isiyotarajiwa na wengi, juzikati abiria mmoja ambaye jina
lake halikuweza kupatikana mkazi wa jijini Dar es Salaam alilazimika
kuendesha daladala baada ya trafiki kumtia nguvuni dereva.
Ilikuwa asubuhi wakati daladala hilo lilipoanza safari yake Kituo cha
Gongo la Mboto kwenda Sinza, kondakta wake aliendelea kuita abiria kwa
muda mrefu licha gari hilo kuwa ‘nyomi’.
Wakati abiria wakimtaka kondakta huyo kuruhusu gari kuondoka, aliwajibu
kwa kebehi kwamba daladala huwa halijai inayojaa ni ndoo ya maji.
Baada ya muda kondakta alimruhusu dereva kuendesha gari, bila kuchelewa
lilianza kushika kasi na abiria wakawa na matagemeo ya kuwahi makazini
mwao.
Basi hilo lililopofika Kituo cha Mombasa, Ukonga askari wa usalama
barabarani aliona jinsi abiria walivyokuwa wakining’inia mlangoni,
akalisimamisha.
Askari alimtaka dereva kutoa faini ya shilingili 20,000 lakini suka
alisema hakuwa na kiasi hicho kwani ndiyo kwanza walianza kazi.
Dereva: Naomba unisamehe afande nakiri nimefanya kosa, kwani ndiyo kwanza naamka hivyo sina kitu kabisa.
Askari: Kama ulilijua hilo kwa nini unaendesha gari huku abiria wakiwa wananing’inia?
Mabishano yalikuwa marefu na kuwafanya abiria kuanza kupiga kelele za
kumtaka dereva kuwapeleka kwani walikuwa wakichelewa kazini.
Baada ya kelele nyingi zisizo na majibu, abiria mmoja aliamua kwenda
kukaa kwenye usukani na kuanza kuliendesha daladala ambalo dereva
alikuwa ameliacha katika ‘sailensi’.
Abiria waliaanza kushangilia kwa kitendo hicho, dereva alianza
kulikimbilia gari hilo na kumuacha askari akiwa ameduwaa asijue la
kufanya.
Dereva alikodi pikipiki na kuanza kulifukuzia daladala hilo na kufanikiwa kulikuta kwenye foleni maeneo ya Vingunguti.
Dereva alianza kumfokea abiria aliyekuwa akiliendesha gari hilo bila
ruhusa yake lakini abiria walionekana kuwa upande wa abira mwenzao kwa
kumshambulia dereva.
like page yetu kwa vituko zaidi