Pages

Wednesday 4 January 2017

Tazameni Mtekelezaji wa Mambo ya Ajabu!

“Simama kimya, uzifikiri [“uzizingatie,” “NW”] kazi za Mungu za ajabu.”—AYUBU 37:14.
1, 2. Ni uvumbuzi gani wa ajabu uliofanywa mwaka wa 1922, nao ulionwaje?
MWAKIOLOJIA mmoja na mheshimiwa mmoja Mwingereza walikuwa wameshirikiana kwa miaka mingi kutafuta hazina. Hatimaye, Novemba 26, 1922, katika makaburi ya mafarao wa Misri kwenye Bonde maarufu la Wafalme, mwakiolojia Howard Carter na Mheshimiwa Carnarvon walipata hazina hiyo—kaburi la Farao Tutankhamen. Walitoboa shimo kwenye mlango uliokuwa umezibwa kabisa kisha Carter akaingiza mshumaa na kuchungulia ndani.

2 Baadaye Carter alisema: “Wakati Mheshimiwa Carnarvon, aliyekuwa na hamu kubwa sana ya kujua yaliyokuwemo ndani, aliponiuliza, ‘Unaona nini humo ndani?’ ningeweza kujibu tu, ‘Naona vitu vya ajabu.’” Ndani ya kaburi hilo kulikuwemo jeneza la dhahabu tupu miongoni mwa vitu vingi vyenye thamani. Labda umeona baadhi ya ‘vitu hivyo vya ajabu’ kwenye picha au kwenye maonyesho katika jumba la makumbusho. Lakini hata vitu hivyo viwe vya ajabu namna gani, yaelekea havina thamani yoyote kwako. Kwa hiyo acheni tuzingatie mambo ya ajabu ambayo bila shaka yanakuhusu na ni yenye thamani kwako.
3. Tutapata wapi habari kuhusu mambo ya ajabu ambayo yanaweza kutunufaisha?
3 Kwa mfano, hebu mfikirie mwanamume aliyeishi karne nyingi zilizopita, mtu mashuhuri kuliko mcheza-sinema, mwanamichezo, mwanasiasa, au mtu yeyote kutoka katika familia ya kifalme. Alisemwa kuwa mkuu sana kuliko watu wote wa upande wa Mashariki. Jina lake ni Ayubu. Kitabu kizima cha Biblia kiliandikwa kumhusu. Hata hivyo, mmoja wa watu walioishi wakati wake, kijana aitwaye Elihu, aliona ni lazima kumsahihisha. Elihu alisema kwamba Ayubu alikuwa akijifikiria mwenyewe na wengine kupita kiasi. Katika Ayubu sura ya 37, twaona ushauri mwingine hususa na wenye hekima, ambao unaweza kutunufaisha sana.—Ayubu 1:1-3; 32:1–33:12.
4. Nini kilichomfanya Elihu atoe himizo lililo kwenye Ayubu 37:14?
4 Watu watatu waliodai kuwa marafiki wa Ayubu walizungumzia kirefu makosa ambayo walidhani Ayubu alikuwa amefanya kwa kuwaza ama kutenda. (Ayubu 15:1-6, 16; 22:5-10) Elihu alisubiri hadi mazungumzo hayo yakaisha. Kisha akaongea kwa hekima na ufahamu wenye kina. Alizungumzia mambo mengi yenye manufaa kubwa, lakini ona wazo hili muhimu: “Sikiliza neno hili, Ee Ayubu; simama kimya, uzifikiri [“uzizingatie,” NW] kazi za Mungu za ajabu.”—Ayubu 37:14.
Aliyezitekeleza Kazi Hizo
5. “Kazi za Mungu za ajabu” ambazo Elihu alirejezea zatia ndani nini?
5 Ona kwamba Elihu hakuwa anadokeza kwamba Ayubu ajizingatie mwenyewe, wala amzingatie yeye Elihu, wala azingatie wanadamu wengine. Kwa hekima Elihu alimhimiza Ayubu—hata sisi pia—azingatie kazi za Yehova Mungu za ajabu. Je, unafikiri usemi “kazi za Mungu za ajabu” watia ndani nini? Isitoshe, kwa nini uzingatie kazi za Mungu ilhali huenda ukawa na mahangaiko kuhusu afya, hali ya kifedha, wakati ujao, familia yako, wafanyakazi wenzako, na majirani? Bila shaka, kazi za ajabu za Yehova Mungu zatia ndani hekima yake na mamlaka yake juu ya uumbaji wote unaotuzunguka. (Nehemia 9:6; Zaburi 24:1; 104:24; 136:5, 6) Ili kuelewa vizuri zaidi jambo hilo, ona yanayosemwa katika kitabu cha Yoshua.
6, 7. (a) Yehova alitekeleza kazi gani za ajabu siku za Musa na Yoshua? (b) Kama ungalishuhudia mojawapo ya kazi hizo wakati wa Musa au wa Yoshua, ungaliitikiaje?
6 Yehova alileta mapigo dhidi ya Misri ya kale kisha akatenganisha maji ya Bahari Nyekundu ili Musa awakomboe Waisraeli wa kale. (Kutoka 7:1–14:31; Zaburi 106:7, 21, 22) Yoshua sura ya 3 inasimulia tukio linalofanana na hilo. Yoshua, mwandamizi wa Musa, alipaswa kuwaongoza watu wa Mungu wavuke mto fulani na kuingia katika Bara Lililoahidiwa. Yoshua alisema: “Jitakaseni; maana kesho BWANA atatenda mambo ya ajabu kati yenu.” (Yoshua 3:5) Mambo gani ya ajabu?
7 Simulizi hilo laonyesha kwamba Yehova alifungua njia katikati ya Mto Yordani ili mamia ya maelfu ya wanaume, wanawake, na watoto wavuke wakitembea pakavu. (Yoshua 3:7-17) Kama tungalikuwa huko na kutazama maji ya mto yakitengana na watu wote hao wakivuka salama, tungaliona utimizo huo kuwa wa ajabu kama nini! Lilionyesha nguvu za Mungu juu ya uumbaji. Hata hivyo, leo hii—nyakati zetu—kuna mambo ya ajabu pia. Ili kuona baadhi ya mambo hayo na kuona ni kwa nini mimi na wewe twapaswa kuyazingatia, ona andiko la Ayubu 37:5-7.
8, 9. Andiko la Ayubu 37:5-7 lazungumzia kazi gani za ajabu na kwa nini tuzifikirie?
8 Elihu alitangaza: “Mungu hunguruma kwa kustaajabisha kwa sauti yake; hufanya mambo makuu, ambayo hatuwezi kuelewa nayo.” Elihu alimaanisha nini aliposema Mungu hufanya mambo “kwa kustaajabisha”? Elihu alikuwa anazungumza juu ya theluji na mvua. Vitu hivyo vingemzuia mkulima asifanye kazi shambani mwake na kumpa wakati na sababu ya kuzizingatia kazi za Mungu. Huenda tusiwe wakulima, lakini sote tunaweza kuathiriwa na mvua na theluji. Ikitegemea tunakoishi duniani, theluji na mvua zaweza kuvuruga shughuli zetu pia. Je, sisi huchukua wakati kutafakari ni nani asababishaye maajabu hayo nayo yanamaanisha nini? Je, umewahi kutafakari juu ya mambo hayo?
9 Kama tusomavyo katika kitabu cha Ayubu sura ya 38, ni jambo lenye kutokeza kwamba Yehova Mungu mwenyewe ana maoni kama hayo kuhusu kutafakari anapomwuliza Ayubu maswali muhimu. Ingawa Muumba wetu alimwuliza Ayubu maswali hayo, ni wazi kwamba yanatuhusu—yanahusu mtazamo wetu, kuwapo kwetu, na wakati wetu ujao. Kwa hiyo, hebu tuchunguze maswali ambayo Mungu aliuliza na kufikiria maana yake, naam, na tufanye yale ambayo andiko la Ayubu 37:14 latuhimiza tufanye.
10. Ayubu sura ya 38 yapasa kuwa na matokeo gani kwetu, nayo yazusha maswali gani?
10 Sura ya 38 yaanza hivi: “BWANA akamjibu Ayubu katika upepo wa kisulisuli, na kusema, Ni nani huyu atiaye mashauri giza kwa maneno yasiyo na maarifa? Basi jifunge viuno kama mwanamume, maana nitakuuliza neno, nawe niambie.” (Ayubu 38:1-3) Utangulizi huo ulimsaidia Ayubu arekebishe maoni yake na kutambua kwamba anasimama mbele za Muumba wa ulimwengu wote, na anawajibika mbele zake. Yafaa sisi na wengine wanaoishi wakati huu tufanye hivyo pia. Kisha, Mungu azungumzia mambo yaleyale ambayo Elihu alikuwa amezungumzia. “Ulikuwa wapi nilipoiweka misingi ya nchi? Haya! sema, kama ukiwa na ufahamu. Ni nani aliyeamrisha vipimo vyake, kama ukijua? Au ni nani aliyenyosha kamba juu yake? Misingi yake ilikazwa juu ya kitu gani? Au ni nani aliyeliweka jiwe lake la pembeni?”—Ayubu 38:4-6.
11. Twapaswa kung’amua nini kutokana na andiko la Ayubu 38:4-6?
11 Ayubu alikuwa wapi, sisi tulikuwa wapi dunia ilipoumbwa? Je, yeyote kati yetu alichora ramani za ujenzi za dunia yetu, na kutumia ramani hiyo kupima vipimo mbalimbali kana kwamba kwa rula? Bila shaka la. Wanadamu hata hawakuwepo wakati huo. Akiifananisha dunia yetu na jengo, Mungu aliuliza hivi: “Ni nani aliyeliweka jiwe lake la pembeni?” Tunajua kwamba dunia imewekwa umbali hususa kutoka kwa jua, umbali unaotuwezesha kuishi na kufurahia maisha. Nayo dunia ina ukubwa ufaao. Kama dunia yetu ingalikuwa kubwa zaidi ya vile ilivyo sasa, gesi ya hidrojeni haingeweza kutoka katika angahewa letu nayo dunia haingekalika. Ni wazi kwamba mtu fulani ‘aliliweka jiwe lake la pembeni’ mahali pafaapo. Je, Ayubu alistahili sifa kwa jambo hilo? Je, sisi twastahili sifa? Au Yehova Mungu ndiye anayestahili sifa?—Mithali 3:19; Yeremia 10:12.
Ni Mwanadamu Gani Awezaye Kutoa Majibu?
12. Swali linalopatikana kwenye Ayubu 38:6 lafanya tufikirie nini?
12 Mungu aliuliza hivi pia: “Misingi yake ilikazwa juu ya kitu gani?” Je, hilo si swali zuri? Huenda twajua nguvu za uvutano, jambo ambalo Ayubu hakujua. Wengi wetu twafahamu kwamba nguvu za uvutano za jua huwezesha dunia idumu mahali ilipo, kana kwamba misingi yake imekazwa. Hata hivyo, je, kuna yeyote kati yetu awezaye kuzielewa kikamili nguvu za uvutano?
13, 14. (a) Ni lazima tukiri nini kuhusu nguvu za uvutano? (b) Tuoneje hali inayokaziwa na andiko la Ayubu 38:6?
13 Kitabu kilichochapishwa hivi majuzi, The Universe Explained, chakiri kwamba ‘watu wengi wanazijua nguvu za uvutano, lakini hawazielewi vizuri kama wanavyoelewa nguvu nyinginezo za asili.’ Kitabu hicho chaendelea kusema: “Yaonekana kwamba nguvu za uvutano husafiri kasi angani, bila kufuata njia yoyote mahususi. Hata hivyo, katika miaka ya majuzi, wanafizikia wameanza kukisia kwamba huenda ikawa nguvu za uvutano husafiri kwa mawimbi ya chembe ndogo ziitwazo graviton . . . Lakini hakuna yeyote aliye na uhakika kwamba chembe hizo zipo.” Hebu wazia hilo lamaanisha nini.
14 Sayansi imepiga hatua kubwa kwa miaka 3,000 tangu Yehova alipomwuliza Ayubu maswali hayo. Hata hivyo, wala sisi wala wataalamu wa fizikia hawawezi kueleza kikamili jinsi nguvu za uvutano zidumishavyo dunia katika mzunguko wake, mahali hasa ipaswapo kuwa ili kutuwezesha kufurahia maisha. (Ayubu 26:7; Isaya 45:18) Kusema hivyo hakudokezi kwamba sote tunahitaji kuanza uchunguzi wenye kina juu ya mambo tusiyoelewa kuhusu nguvu za uvutano. Hata hivyo, kuzingatia hata sehemu hii moja tu ya kazi za Mungu za ajabu kwapasa kuathiri maoni yetu kumhusu. Je, unastaajabia hekima yake na ujuzi wake, na je, unaelewa ni kwa nini twahitaji kujifunza mengi zaidi juu ya mapenzi yake?
15-17. (a) Andiko la Ayubu 38:8-11 lakazia nini na linazusha maswali gani? (b) Twapaswa kukiri nini juu ya yale tunayojua kuhusu bahari na mahali zilipo duniani?
15 Muumba aliendelea kuuliza hivi: “Ni nani aliyeifunga bahari kwa milango, hapo ilipofurika kana kwamba imetoka tumboni. Nilipolifanya wingu kuwa vazi lake, na giza zito kuwa nguo ya kuifungia, nikaiagiza amri yangu; nikaiwekea makomeo na milango, nikasema, Utafika mpaka hapa, lakini hutapita, na hapa mawimbi yako yanyetayo yatazuiliwa?”—Ayubu 38:8-11.
16 Kufungwa kwa bahari kwahusisha mabara, bahari, na mawimbi. Mwanadamu amechunguza na kuchanganua vitu hivyo kwa muda mrefu kadiri gani? Amefanya hivyo kwa maelfu ya miaka na kwa makini zaidi hasa katika karne iliyopita. Unaweza kuwazia kwamba kufikia sasa lazima mwanadamu awe anajua mambo mengi ambayo anapaswa kujua kuhusu vitu hivyo. Lakini, katika mwaka huu wa 2001, ungepata habari gani za karibuni zaidi kama ungechunguza juu ya vitu hivyo kwenye maktaba kubwa au kwenye Internet yenye uwezo mkubwa wa kufanya utafiti?
17 Kichapo kimoja maarufu cha marejezo, chakiri hivi: ‘Ni vigumu sana kwa wanasayansi kuchunguza kikamili au kutoa nadharia inayoweza kueleza ni kwa nini mabara, bahari na uumbaji mwingine, upo mahali ulipo.’ Baada ya kusema hayo, ensaiklopidia hiyo ilitoa mambo manne ambayo yawezekana yalisababisha hali hiyo, lakini ikasema kwamba mambo hayo ni “baadhi ya zile nadharia tete nyingi.” Huenda ukafahamu kwamba usemi nadharia tete “wamaanisha uthibitisho usiotosha ambao watoa ufafanuzi uwezao kubadilika.”
18. Andiko la Ayubu 38:8-11 lafanya tufikie mkataa gani?
18 Je, mambo hayo hayakazii kwamba maswali tusomayo kwenye Ayubu 38:8-11 yaliulizwa wakati ufaao? Bila shaka, hatuwezi kupokea sifa kwa kuwa sio sisi tulioviweka vitu hivyo mahali vilipo duniani. Hatukuuweka mwezi mahali ulipo ili nguvu zake za uvutano zisaidie kutokeza mawimbi ambayo kwa kawaida hayaharibu mwambao wala kutuathiri sisi binafsi. Tunajua kwamba Mtekelezaji wa mambo ya ajabu ndiye aliyefanya hayo yote.—Zaburi 33:7; 89:9; Mithali 8:29; Matendo 4:24; Ufunuo 14:7.
Mpe Yehova Sifa Anayostahili
19. Semi za kishairi kwenye Ayubu 38:12-14 zafanya tuzingatie mambo gani halisi?
19 Mzunguko wa dunia unaorejezewa kwenye andiko la Ayubu 38:12-14 haukutokezwa na wanadamu. Mzunguko huo wa dunia husababisha mapambazuko ambayo mara nyingi huvutia kwa uzuri. Jua lichomozapo, vitu vilivyomo katika dunia yetu huonekana vizuri zaidi na zaidi kama vile alama kwenye udongo laini. Tunapozingatia kwa kiasi kidogo mwendo wa dunia twastaajabu kuona kwamba haizunguki kwa kasi sana, jambo ambalo kama tujuavyo lingeleta madhara. Wala dunia haizunguki polepole sana hivi kwamba mchana na usiku zawa ndefu sana. Jambo hilo laweza kusababisha joto na baridi zinazopita kiasi na kufanya wanadamu wasiweze kuishi. Kusema kweli, yatupasa kufurahi kwamba Mungu ndiye aliyeanzisha mwendo wa mzunguko huo, wala si wanadamu fulani.—Zaburi 148:1-5.
20. Ungejibuje maswali yaliyoulizwa kwenye Ayubu 38:16, 18?
20 Sasa, hebu wazia Mungu akikuuliza maswali zaidi: “Je! umeziingia chemchemi za bahari, au umetembea mahali pa siri pa vilindi?” Hata mtaalamu wa mambo ya bahari hangeweza kutoa jibu kamili! “Umeyafahamu mapana ya dunia? Haya! sema, ikiwa unayajua hayo yote.” (Ayubu 38:16, 18) Je, umezuru na kutembelea sehemu zote za dunia au angalau sehemu nyingi za dunia? Kutembelea sehemu nzuri mbalimbali na kuona maajabu ya dunia yetu kungechukua muda mrefu kadiri gani? Nao ungekuwa wakati mzuri kama nini!
21. (a) Maswali yaliyoulizwa kwenye Ayubu 38:19 yanaweza kutokeza maoni gani ya kisayansi? (b) Mambo halisi kuhusu nuru yapasa kutuchochea tufanye nini?
21 Pia, tazama maswali mazito katika Ayubu 38:19: “Iko wapi njia ya kuyafikia makao ya nuru? Na giza pia, mahali pake ni wapi?” Huenda ikawa wajua kwamba kwa muda mrefu, wanasayansi walidhani kwamba nuru husafiri kama wimbi, kama viwimbi tuonavyo kwenye kidimbwi. Kisha katika mwaka wa 1905, Albert Einstein akaeleza kwamba nuru ni kama chembechembe za nishati. Je, ufafanuzi wa Einstein ulitoa jibu? Ensaiklopidia ya karibuni iliuliza hivi: “Je, nuru ni wimbi au ni chembechembe?” Nayo yajibu hivi: “Yaonekana kwamba, [nuru] haiwezi kuwa [wimbi na wakati uleule ikawa chembechembe] kwa sababu vitu hivyo viwili vyatofautiana sana. Jibu lifaalo kabisa ni kwamba nuru si wimbi wala si chembechembe.” Hata hivyo, ingawa mwanadamu hawezi kufafanua kikamili kazi hizo za Mungu jua bado laendelea kupasha joto (kwa njia ya moja kwa moja au kwa njia nyingineyo). Twapata chakula na oksijeni kwa sababu mimea hupata nuru. Twaweza kusoma, kuona nyuso za wapendwa wetu, kutazama machweo, na kadhalika. Tufanyapo hivyo, je, hatupaswi kushukuru kwa sababu ya kazi za Mungu za ajabu?—Zaburi 104:1, 2; 145:5; Isaya 45:7; Yeremia 31:35.
22. Daudi aliyeishi zamani alizionaje kazi za Mungu za ajabu?
22 Je, tunatafakari kazi za Yehova za ajabu kusudi tu tustaajabu au kuduwaa? La, hasha. Mtunga-zaburi aliyeishi zamani alikiri kwamba haiwezekani kufahamu au kueleza kazi zote za Mungu. Daudi aliandika: “Ee BWANA, Mungu wangu, umefanya kwa wingi miujiza yako; [“kazi zako za ajabu,” NW] . . . Kama ningependa kuyatangaza na kuyahubiri, ni mengi sana hayahesabiki.” (Zaburi 40:5) Bila shaka Daudi hakumaanisha kwamba hangezungumza kuhusu kazi hizo zenye kuvutia. Daudi alithibitisha hilo kwa azimio lake linalotajwa kwenye Zaburi 9:1: “Nitamshukuru BWANA kwa moyo wangu wote; nitayasimulia matendo yako yote ya ajabu.”
23. Unazionaje kazi za Mungu za ajabu, na unaweza kuwasaidiaje wengine?
23 Je, hatupaswi kuchochewa vivyo hivyo? Je, kustaajabia kwetu kazi za Mungu zenye kuvutia hakupasi kutuchochea kuzungumza juu yake, juu ya yale ambayo amefanya, na yale ambayo bado atafanya? Jibu ni wazi—tunapaswa ‘kuwahubiri mataifa habari za utukufu wake, na watu wote habari za maajabu yake.’ (Zaburi 96:3-5) Naam, tunaweza kuonyesha uthamini wetu wenye unyenyekevu kwa kazi za Mungu za ajabu kwa kujulisha wengine yale ambayo tumejifunza kumhusu. Hata wawe walilelewa katika jamii ambayo haimtambui Muumba, huenda maneno yetu yenye kujenga na yenye kuelimisha yakawaamsha fikira watambue kuna Mungu. Isitoshe, huenda yakawachochea kutaka kujifunza na kumtumikia yule ambaye ‘aliumba vitu vyote,’ Yehova, Mtekelezaji wa kazi za ajabu.—Ufunuo 4:11.
Ungejibuje?
• Himizo kwenye Ayubu 37:14 lakufanya ufikirie kazi gani za Mungu?
• Ni baadhi ya mambo gani ambayo yamekaziwa kwenye sura za 37 na 38 za kitabu cha Ayubu ambayo sayansi haiwezi kueleza kikamili?
• Unahisije kuhusu kazi za Mungu za ajabu na jambo hilo lakuchochea ufanye nini?
[Picha katika ukurasa wa 7]
Ni nani aliyeifunga bahari na kuiweka mahali pake?
[Picha katika ukurasa wa 7]
Ni nani ambaye amezuru sehemu zote zenye kuvutia duniani, ambazo Mungu aliumba?

No comments:

Post a Comment

 

Blogger news

Blogroll

LIKE PAGE YETU KWA HABARI ZA KILA WAKATI

Receive all updates via Facebook. Just Click the Like Button Below

Powered By Blogger Widgets