Pages

Saturday 18 April 2015

Ukweli Kuhusu Mbingu

WATU fulani wanafikiri kwamba hatuwezi kujua ukweli kuhusu mbingu kwa sababu hakuna mtu ambaye ameshuka kutoka huko ili atueleze mambo ya mbinguni. Labda wamesahau kwamba Yesu alisema hivi: “Nimeshuka kutoka mbinguni.” (Yohana 6:38) Pia, aliwaambia hivi viongozi fulani wa kidini: “Ninyi mnatoka kwenye makao ya chini; mimi ninatoka kwenye makao ya juu.” (Yohana 8:23) Yesu alisema nini kuhusu mbingu?

Yesu alituhakikishia kwamba Yehova anaishi mbinguni. Alimwita Mungu “Baba yangu aliye mbinguni.” (Mathayo 12:50) Lakini Yesu alitumia neno “mbinguni” kwa njia mbalimbali. Kwa mfano, aliliita angahewa la dunia ‘mbingu’ aliposema hivi: “Waangalieni kwa makini ndege wa mbinguni.” (Mathayo 6:26) Hata hivyo, Yehova anaishi juu zaidi ya angahewa la dunia. Biblia inasema hivi: “Kuna Yeye anayekaa juu ya mviringo wa dunia.”—Isaya 40:22.
Je, ‘Baba aliye mbinguni’ anaishi kati ya nyota? Sayari na nyota kwa ujumla zinaitwa pia “mbingu” katika Maandiko Matakatifu. Kwa mfano, mtunga-zaburi mmoja aliandika hivi: “Ninapoziona mbingu zako, kazi za vidole vyako, mwezi na nyota ambazo umetayarisha, mwanadamu anayeweza kufa ni nini hivi kwamba umweke akilini?”—Zaburi 8:3, 4.
Hapana, Yehova Mungu hawezi kuishi ndani ya ulimwengu ambao aliumba, kama vile tu seremala asivyoweza kuishi ndani ya kabati alilotengeneza. Hivyo, Mfalme Sulemani alipoweka hekalu wakfu kwa Yehova huko Yerusalemu, alisema hivi: “Je, kweli Mungu atakaa duniani? Tazama! Mbingu, ndiyo, mbingu za mbingu, haziwezi kukutosha; jinsi gani basi, nyumba hii ambayo nimeijenga!” (1 Wafalme 8:27) Ikiwa Yehova haishi katika mbingu zinazoonekana, basi anaishi katika mbingu gani?
Ingawa wanadamu wamechunguza mbingu zenye nyota kwa darubini zenye nguvu na hata wengine wameenda kwenye anga za juu, maneno haya ya Biblia bado ni ya kweli: “Hakuna mwanadamu ambaye amemwona Mungu wakati wowote.” (Yohana 1:18) Yesu alionyesha sababu aliposema hivi: “Mungu ni Roho.”—Yohana 4:24.
Roho ni aina ya uhai ambao ni bora kuliko uhai wa mwanadamu. Mwili wa roho hauna vitu kama vile nyama na damu ambavyo vinaweza kuonekana na kuguswa na wanadamu. Kwa hiyo, Yesu aliposema kwamba alikuwa anaishi kando ya Baba yake “mbinguni,” alimaanisha kwamba alikuwa na uhai wenye utukufu kuliko uhai wowote duniani. (Yohana 17:5; Wafilipi 3:20, 21) Katika Biblia, makao hayo ya roho ambamo Yesu alikuwa anaishi pamoja na Baba yake yanaitwa ‘mbingu.’ Ni makao ya aina gani? Ni kazi gani inayofanywa huko?
Mahali pa Utendaji Wenye Furaha
Biblia inaonyesha kwamba mbingu ni mahali penye utendaji mwingi. Inataja mamia ya mamilioni ya viumbe waaminifu wa roho ambao wanaishi huko. (Danieli 7:9, 10) Kila mmoja wa viumbe hao wa roho ana utu wa kipekee. Tunajua hivyo jinsi gani? Kati ya viumbe wote duniani, hakuna viumbe wawili walio hai ambao wanafanana kabisa, kwa hiyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba viumbe walio mbinguni pia wana utu tofauti-tofauti. Kwa kushangaza, viumbe hao wote wa mbinguni wanafanya kazi pamoja kwa umoja, tofauti sana na wanadamu ambao kwa kawaida hawashirikiani vizuri leo.
Ona jinsi Biblia inavyoeleza kuhusu utendaji wa mbinguni. “Mbarikini Yehova, enyi malaika zake, mlio na uwezo katika nguvu, mnaolitenda neno lake, kwa kuisikiliza sauti ya neno lake. Mbarikini Yehova, enyi majeshi yake yote, enyi wahudumu wake, mnaofanya mapenzi yake.” (Zaburi 103:20, 21) Hivyo, kuna kazi nyingi sana inayofanywa mbinguni. Tunaweza kuwa na hakika kwamba ni kazi inayoridhisha.
Malaika wamekuwa wakimtumikia Yehova kwa furaha kwa miaka mingi sana, hata kabla dunia haijaumbwa. Maandiko yanasema kwamba Yehova alipoweka msingi wa dunia, wana wa Mungu ‘walipiga vigelegele pamoja kwa shangwe’ na “wakaanza kupaaza sauti kwa kushangilia.” (Ayubu 38:4, 7) Hata mwana mmoja wa kimbingu wa Mungu alipata pendeleo la kufanya kazi pamoja na Mungu katika kuumba vitu vingine vyote. (Wakolosai 1:15-17) Huenda maelezo hayo yenye kuvutia kuhusu utendaji wenye furaha mbinguni yakafanya ujiulize maswali kuhusu mbingu na wanadamu.
Je, Wanadamu Walikusudiwa Kwenda Mbinguni?
Kwa kuwa malaika walikuwa wanamtumikia Mungu mbinguni kabla ya dunia kuumbwa, inaonekana kwamba mwanamume na mwanamke wa kwanza hawakuumbwa ili wajaze mbingu. Badala yake, Mungu aliwaambia hivi wenzi hao wawili wa kwanza: “Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia.” (Mwanzo 1:28; Matendo 17:26) Adamu alikuwa wa kwanza kati ya aina mpya ya uhai wa kidunia. Angeweza kumjua Mungu na kumtumikia kwa uaminifu. Angekuwa baba ya wanadamu ambao wangeishi duniani. “Mbingu ni mbingu za Yehova, bali dunia amewapa wana wa binadamu.”—Zaburi 115:16.
Kwa kawaida, watu hawataki kufa; wanadamu hawakuumbwa ili wafe. Mungu alimwambia Adamu kwamba kifo kingekuwa tu adhabu ya kutotii. Ikiwa Adamu angetii, hangekufa kamwe.—Mwanzo 2:17; Waroma 5:12.
Basi, haishangazi kwamba Mungu hakumwambia Adamu lolote kuhusu kwenda mbinguni. Kwa hiyo, dunia haikukusudiwa kuwa uwanja wa mazoezi ambapo watu wangejaribiwa ili kuona ikiwa wanastahili kuishi mbinguni. Mwanadamu aliumbwa ili aishi milele duniani, na bado kusudi hilo la Mungu litatimizwa. Biblia inaahidi kwamba “waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.” (Zaburi 37:29) Ni wazi kwamba tangu mwanzoni wanadamu hawakukusudiwa kwenda mbinguni. Basi, kwa nini Yesu aliwaahidi mitume wake kwamba wangeishi mbinguni? Je, Yesu alimaanisha kwamba watu wote wazuri wataenda mbinguni?

No comments:

Post a Comment

 

Blogger news

Blogroll

LIKE PAGE YETU KWA HABARI ZA KILA WAKATI

Receive all updates via Facebook. Just Click the Like Button Below

Powered By Blogger Widgets