Pages

Friday 21 August 2015

Viumbe wa ajabu wa baharini








WATU wengi wanadhani kuwa utafiti kuhusiana na wanyama umekamilika. Lakini ukweli ni kuwa bado kuna maswali mengi sana kuhusiana na maisha ya wanyama mbalimbali ambayo hayajapatiwa majibu.
Ndio maana kila kukicha unajitokeza ugunduzi mwingine mpya ambao mara nyingi unawaacha watafiti vinywa wazi lakini baadaye unatoa mwanga wa masuala kadhaa waliyokuwa hawayaelewi awali.
Mathalani, tunafahamu visa kadhaa vya watoto kuzaliwa wakiwa wameungana. Lakini hivi karibuni watafiti wa huko Mexico walimgundua nyangumi wa kijivu walioungana.
Inaaminika kuwa hili ni tukio la kwanza duniani la kupatikana kwa nyangumi pacha wa aina hii walioungana.
Zipo taarifa nyingine za nyangumi walioungana lakini taarifa hizo hazijafanywa kuwa rasmi. Ndio maana watu wengi, wakiwamo watafiti wanaamini kuwa hili litakuwa tukio la kwanza na la kuweka rekodi kuhusiana na nyangumi pacha wa kijivu waliungana.
Hata hivyo, kwa bahati mbaya sana, pacha hao waligunduliwa wakiwa tayari wameshafariki. Inaaminika kuwa walifariki hata kabla hawajazaliwa.
Inaaminika kuwa ilikuwa ni mimba iliyoharibika kwa sababu mzoga huo ulikuwa na urefu wa futi saba wakati nyangumi anazaliwa akiwa na urefu wa futi kati ya 12 na 16.
Mtafiti mmoja kutoka Marekani Alisa Schulman Janiger, anasema uchunguzi wake ulibaini kuwa pacha hao walikuwa hawajafikia hatua ya kuzaliwa. Lakini pia anaamini kuwa kuna uwezekano wa watoto hao kuuawa na mama yao.
Pamoja na kuwa pacha hao wa nyangumi walioungana waligunduliwa wakiwa wameshakufa, lakini mabaki yake yalikusanywa na kuhifadhiwa kwa ajili ya utafiti wa kina.
Ni kawaida kwa nyangumi wa kijivu kufika katika eneo hilo la Scammon na maeneo mengine yanayofanana na hilo katika ufukwe wa Baja huko California, baada ya safari ya karibu kilometa 6,000 kutoka maeneo ya Arctic ambako huishi kwa kipindi kirefu.
Katika safari hii kuelekea maeneo ya kusini ndipo wanapozaa katika maeneo hayo ya lagoon na kuwatunza watoto wao kwa wiki kadhaa kabla hawajaanza safari ya kurejea kaskazini ambako ndiko kwenye makazi yao katika bahari za Bering na Chukchi.
Watoto wengi huzaliwa katika wiki ya mwisho ya Disemba na wiki mbili za kwanza za Januari kila mwaka. Kwa mujibu wa taasisi  ya NOAA, idadi ya nyangumi wa kijivu katika bahari ya Pacific ni kama 21,000.
Ukiachana na nyangumi hawa walioungana ambao wameleta mwanga mpya katika sayansi ya viumbe wa baharini, pia kuna tukio jingine la kuvuliwa kwa kiumbe mwingine mkubwa katika eneo la bahari ya Florida.
Kutokana na ukubwa wake ilikuwa ni vigumu kufahamu hasa yeye ni samaki wa aina gani ingawa utafiti wa awali unaonesha kuwa anaweza kuwa papa.
Alivuliwa na mvuvi Mark Quartiano ambaye amebatizwa jina la mvua papa kutokana na umahiri wake wa kuvua samaki aina ya papa. Mark tayari ameshakamata maelfu ya samaki hao, lakini hii ilikuwa ni mara yake ya kwanza kumvua kiumbe wa ajabu kama huyo aliyekuwa na uzito wa paundi 800 katika maeneo ya fukwe za Miami.
Mark mwenyewe alionyesha kushangazwa na kiumbe hicho ambacho anasema ukubwa wake unamfanya afanane na mnyama mkubwa wa kale aitwaye dinosaria.
Mark anasema awali alidhani kuwa jina la kisayansi la papa aliyemvua ni Dactylobatus Clarkii, lakini alipotafuta katika mtandao wa intanet kuhusiana na samaki wa jamii hiyo alipata taarifa kiduchu.
Hata hivyo, siku chache baadaye, baada ya kuona picha za samaki huyo wa ajabu, Mtafiti George H. Burgess kutoka Florida Museum of Natural History alimtambua samaki huyo kuwa ni jamii ya Stingray ambaye jina lake la kisayansi ni Dasyatis Centroura.
Samaki huyo hupenda kuishi katika kilindi kirefu cha maji katika eneo la bonde la ufa la baharini huko mashariki mwa Marekani kati ya maeneo la Carolina na Uruguay, na pia mashariki mwa bahari ya Atlantic.
“Kwa sababu wavuvi wengi hawajihusishi na kuvua katika vina virefu vya maji ndio maana samaki huyu hajawahi kuonekana mara nyingi. Lakini, wavuvi wanaotumia meli kubwa pamoja na watafiti wanaofika katika maeneo ya chini ya bahari wamekuwa wakiwanasa samaki hawa.
“Kwa hakika samaki mkubwa kama huyu anahitaji vifaa maalum vya uvuvi ili uweze kumuibua hadi juu ya maji. Hawapambani sana wanapokamatwa lakini ni wazito mno,” anasema.
Mark aliyekuwa akivua huku akipigwa picha na timu ya watengeneza vipindi vya runinga kutoka Japani, alikuwa ameishusha ndoano yake hadi chini kabisa ya eneo hilo la maji. Punde, mshipi ulianza kuchezacheza kuashiria kuwa ndoano ilikuwa imenasa kitu.
“Nilikuwa ninavua kwenye kina cha kama futi 500 hivi na wao walikuwa wakichukua picha kwa ajili ya kutengeneza kipindi vya televisheni. Kwa bahati nzuri nikamnasa papa mkubwa mno na kutokana na ukubwa wake ilituchukua zaidi ya saa nne kumuibua juu ya maji.
 Kwanza nikadhani kuwa ni jamii ya papa kwa sababu jinsi alivyokuwa akipambana wakati wa kumvuta ni kama ambavyo papa anafanya,” anasema Mark.
Mmoja wa watengeneza filamu hao alikuwa na vifaa vya kupigia mbizi na alikwenda chini ya maji kurekodi tukio la kukamatwa kwa samaki huyo.
Mark anabainisha kuwa walipomfikisha juu ya maji, watengeneza filamu hao walimwinua na kumning’iniza kwa dakika kama nne hivi huku wakimpiga picha na kisha kumuachia. Anaamini kuwa kulingana na ukubwa wake, alikuwa na uzito unaofikia paundi 800.

No comments:

Post a Comment

 

Blogger news

Blogroll

LIKE PAGE YETU KWA HABARI ZA KILA WAKATI

Receive all updates via Facebook. Just Click the Like Button Below

Powered By Blogger Widgets