Pages

Sunday 23 August 2015

Ulimwengu Uliojaa Maajabu

MIAKA 100 hivi iliyopita, wanasayansi waliamini kwamba ulimwengu mzima unapatikana katika kikundi chetu cha nyota cha Kilimia. Hata hivyo, kwa sababu ya maendeleo makubwa ya astronomia, fizikia, na tekinolojia katika karne ya 20 wanasayansi wamegundua ukubwa halisi wa ulimwengu. Baadhi ya mambo ambayo wamegundua yamewanyenyekeza. Kwa mfano, katika miaka ya hivi karibuni wataalamu wa kuchunguza nyota wamegundua kwamba hawajui kile kinachofanyiza zaidi ya asilimia 90 ya ulimwengu. Isitoshe, ugunduzi ambao umewafanya wafikie mkataa huo umewaacha wanasayansi wakijiuliza ikiwa kweli wanaelewa kanuni za msingi za fizikia. Maswali kama hayo si mageni.

Kwa mfano, karibu na mwisho wa karne ya 19, wanafizikia waliona jambo lisilo la kawaida kuhusu mwendo wa nuru. Waligundua kwamba kwa maoni ya mtazamaji, nuru husonga kwa mwendo uleule haidhuru mtazamaji anasonga kwa kasi kadiri gani. Lakini hilo lilionekana kuwa halipatani na akili! Tatizo hilo lilishughulikiwa mnamo 1905 katika nadharia ya pekee ya Albert Einstein kuhusu uwiano, ambayo ilisema kwamba umbali, wakati, na uzito hubadilika-badilika. Kisha katika mwaka wa 1907, baada ya kupata wazo jipya ambalo aliliita “wazo lenye kufurahisha zaidi maishani mwangu,” Einstein alianzisha nadharia ya uwiano ambayo alichapisha mnamo 1916. Katika nadharia hiyo ya pekee alieleza jinsi nguvu za uvutano, anga za juu, na wakati zinavyoshirikiana na akaboresha maoni ya Isaac Newton.
Ulimwengu Unaopanuka
Kwa kutegemea uthibitisho uliokuwapo wakati huo, Einstein aliamini kwamba ulimwengu unadumu jinsi ulivyo, haupanuki wala kupungua. Hata hivyo, mtaalamu wa nyota kutoka Marekani, Edwin Hubble, mnamo 1929, alionyesha uthibitisho kwamba ulimwengu unapanuka.
Pia Hubble alieleza kuhusu sehemu zenye ukungu unaong’aa angani usiku ambazo kwa muda mrefu zilizoitwa nebula kwa sababu zilionekana kama mawingu ya gesi. Lakini je, mawingu hayo yote yalikuwa katika kundi letu la nyota, au yalikuwa nje kama mtaalamu wa nyota Mwingereza Sir William Herschel (1738-1822) alivyodokeza zaidi ya karne moja mapema?
Hubble alipokadiria kwa mara ya kwanza umbali kutoka duniani hadi kwenye wingu moja kati ya hayo linaloitwa Great Nebula katika kundi la nyota la Andromeda, alifikia mkataa kwamba mawingu hayo yalikuwa kundi la nyota lililo umbali wa miaka milioni moja ya nuru. Hilo lilimaanisha kwamba mawingu hayo yako mbali sana na kikundi cha nyota cha Kilimia kilicho na kipenyo cha miaka 100,000 “tu” ya nuru. Hubble alipopima umbali kutoka duniani hadi kwenye mawingu mengine, alianza kugundua ukubwa usio na kifani wa ulimwengu na akaanzisha mabadiliko makubwa katika astronomia na kosmolojia.*
Muda mfupi baada ya hapo ndipo Hubble alitambua kwamba ulimwengu unapanuka, kwa sababu aliona makundi ya nyota ya mbali yakisonga mbali zaidi na dunia. Pia alitambua kwamba kadiri kundi la nyota lilivyokuwa mbali zaidi ndivyo lilivyosonga mbali kwa kasi zaidi. Maoni hayo yanaonyesha kwamba ulimwengu unapanuka zaidi kila siku. Hubble alipochapisha ugunduzi wake mnamo 1929, alifungua njia kwa ajili ya ukuzi wa nadharia iliyosema kwamba ulimwengu ulitokezwa na mlipuko mkubwa uliotokea kwa aksidenti miaka bilioni 13 hivi iliyopita. Lakini bado kuna mambo mengi zaidi ya kujifunza.
Unapanuka Upesi Kadiri Gani?
Tangu wakati wa Hubble, wataalamu wa nyota wamekuwa wakijaribu kupima kwa usahihi wawezavyo ni kwa kadiri gani ulimwengu unazidi kupanuka. Kwa nini vipimo hivyo ni muhimu sana? Ikiwa wataalamu wa nyota wangeweza kupima ni kwa kadiri gani ulimwengu unapanuka, wangetumia vipimo hivyo kukadiria ulimwengu ulitokea lini. Isitoshe, mwendo wa upanuzi unaweza kuathiri sana wakati ujao. Kwa njia gani? Kwa mfano, inafikiriwa kwamba ikiwa ulimwengu unapanuka polepole sana, huenda nguvu za uvutano zikazidi mwendo wa kupanuka na kufanya kila kitu kiangamie! Lakini ikiwa unapanuka haraka sana, huenda ukapanuka milele na sehemu zote kusambaratika.
Ingawa vipimo sahihi zaidi vimesaidia kujibu maswali fulani, maswali mengine yamezushwa—maswali yanayofanya tutilie shaka jinsi tunavyoelewa mata na kani za asili za msingi.
Nishati Isiyoonekana na Mata Nyeusi
Mnamo 1998, watafiti wanaochunguza nuru kutoka katika nyota inayolipuka waligundua kwamba ulimwengu unapanuka kwa kasi zaidi.* Mwanzoni, wanasayansi walikuwa na shaka, lakini uthibitisho zaidi ulipatikana. Walitaka kujua ni nishati ya aina gani iliyokuwa ikifanya ulimwengu upanuke kwa kasi zaidi. Kwanza, ilipingana na nguvu za uvutano; na pili, haikupatana na nadharia zozote za kisasa. Kwa kufaa, nishati hiyo imesemwa kuwa ni nishati isiyoonekana na inafanyiza karibu asilimia 75 ya ulimwengu wetu!
Hata hivyo, nishati isiyoonekana si kitu pekee kisichoonekana ambacho kimegunduliwa katika siku za karibuni. Kitu kingine kiligunduliwa katika miaka ya 1980 wataalamu wa nyota walipochunguza vikundi kadhaa vya nyota. Vikundi hivyo vya nyota, na vilevile kikundi chetu, vilionekana vinazunguka kwa kasi sana hivi kwamba haviwezi kushikamana. Basi uthibitisho unaonyesha kwamba mata fulani inatoa nguvu za uvutano zinazofanya vishikamane. Lakini hiyo ni aina gani ya mata? Kwa sababu wanasayansi hawajui mata hiyo, waliiita mata nyeusi, kwa kuwa haifyonzi, haitoi, au kutokeza kiasi fulani cha mnururisho.* Kuna kiasi gani cha mata nyeusi? Makadirio yanaonyesha kwamba huenda ni asilimia 22 au zaidi ya ulimwengu.
Fikiria hili: Kulingana na makadirio ya sasa, mata ya kawaida inafanyiza asilimia 4 hivi ya ulimwengu. Inaonekana kwamba mata nyeusi na nishati isiyoonekana vinafanyiza sehemu iliyobaki. Hivyo, asilimia 95 hivi ya ulimwengu ni fumbo!*
Jitihada Zisizo na Mwisho
Sayansi hutafuta majibu, lakini mara nyingi majibu yanatokeza maswali zaidi. Hilo linafanya tukumbuke maneno haya muhimu yaliyo yalioandikwa katika kitabu cha Biblia cha Mhubiri 3:11: “[Mungu] amefanya kila kitu kiwe chenye kupendeza kwa wakati wake. Tena wakati usio na kipimo ameuweka ndani ya moyo wao, ili mwanadamu asiweze kugundua kazi ambazo Mungu wa kweli amefanya tangu mwanzo mpaka mwisho.”
Bila shaka, sasa tunaweza kujifunza mambo machache tu katika maisha yetu mafupi, na ujuzi huo unabadilika-badilika. Lakini hali hiyo ni ya muda tu, kwa kuwa Mungu amekusudia kuwapa wanadamu waaminifu maisha yasiyo na mwisho katika Paradiso duniani ambapo wanaweza kuchunguza uumbaji wake milele na hivyo kupata ujuzi wa kweli.—Zaburi 37:11, 29; Luka 23:43.
Hivyo, hatuhitaji kuogopa kwamba ulimwengu utaangamia. Sayansi imefanya tujue mambo machache tu, lakini Muumba anajua mambo yote.—Ufunuo 4:11.
[Maelezo ya Chini]
Astronomia ni elimu inayohusu nyota, sayari, na mata ulimwenguni. Kosmolojia ni kitengo fulani cha astronomia, “elimu ya muundo na ukuzi wa ulimwengu na nguvu zinazotenda ndani yake,” kinasema kitabu The World Book Encyclopedia. “Wanakosmolojia wanajaribu kueleza jinsi ulimwengu ulivyotokea, mambo ambayo yametukia tangu ulipotokea, na mambo yatakayoupata wakati ujao.”
Nyota zinazolipuka zinaitwa supernova aina ya 1a na zinaweza kung’aa kama jua bilioni moja kwa muda mfupi. Wataalamu wa nyota wanatumia nyota hizo kama kiwango cha kupimia.
Wazo la kwamba kuna mata nyeusi lilianzishwa katika miaka ya 1930 na likathibitishwa katika miaka ya 1980. Leo wataalamu wa nyota wanapima kiasi cha mata nyeusi katika vikundi vingi vya nyota kwa kuchunguza jinsi vikundi hivyo vinavyopinda nuru kutoka kwa vitu vilivyo mbali.
Mwaka wa 2009 umeitwa “Mwaka wa Kimataifa wa Utaalamu wa Nyota,” na ni mwaka wa 400 tangu darubini ya kwanza ya nyota kutumiwa na Galileo Galilei.

No comments:

Post a Comment

 

Blogger news

Blogroll

LIKE PAGE YETU KWA HABARI ZA KILA WAKATI

Receive all updates via Facebook. Just Click the Like Button Below

Powered By Blogger Widgets